Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, February 23, 2013

FAGIO LA CHUMA LA MWAKYEMBE LAPANDISHA MAPATO BANDARI YA DAR ES SALAAM .



Meli zinapakua makontena katika bandari ya Dar es Salaam tarehe 29 Disemba, 2012. [Deodatus Balile/Sabahi]

Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) imeongeza ukusanyaji wa mapato katika bandari ya Dar es Salaam kutoka shilingi bilioni 28 mwezi Novemba hadi shilingi bilioni 50 (dola milioni 18 hadi dola milioni 31) katika mwezi wa Disemba, kufuatiakusimamishwa kwa muda maofisa 16 wa bandari wanaotuhumiwa kwa mwenendo usiofaa.
Maofisa hao wa bandari, wakiwemo wakurugenzi wa ngazi za juu, walisimamishwa kwa muda mwezi Disemba baada ya Wizara ya Usafirishaji kuanzisha uchunguzi wa ndani kwa lengo la kutoa mwitikio wa malalamiko ya wateja kuhusu kucheleweshwa katika bandari hiyo, kwa mujibu wa Waziri wa Usafirishaji Harrison Mwakyembe.
Maofisa wa bandari wengine wasiopungua sita walisimamishwa mwezi Agosti. Uchunguzi huo, ambao bado unaendelea, uligundua kuwa waajiriwa wa bandari walibadilisha mwelekeo wa biashara kutoka katika bandari kwenda kwa kampuni ndogo za usafirishaji na utoaji mizigo wanazomiliki, ukiukaji wa moja kwa moja wa mkataba wao wa ajira.
"Wateja wanakimbia bandari yetu kwa sababu ya ucheleshaji wa kukusudia unaofanywa na waajiriwa wasio na maadili ambao wanaongeza gharama za kufanya biashara," Mwakyembe aliiambia Sabahi. "Hii ni kinyume na mikataba yao ya ajira na wana mgongano wa maslahi na mwajiri wao [serikali]."
Miongoni mwa viongozi wa bandari wa ngazi ya juu waliosimamishwa ni Mkurugenzi Mkuu wa TPA Ephraim Mgawe, Mkurugenzi wa Mipango Florence Nkya, Mkurugenzi wa Uhandisi Bakari Kilo, Mkurugenzi wa Mifumo ya Utawala Maimuna Mrisho, Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Ayub Kamili, Naibu Mkurugenzi Mkuu Hamad Koshyuma, Naibu Mkurugenzi Mkuu Julius Fuko, na Meneja wa Bandari Cassian Ng'amilo.
Mashtaka rasmi bado hayajatolewa dhidi ya viongozi waliosimamishwa na bado hawajajibu tuhuma zozote hadharani. Mwakyembe alisema Bodi ya Wakurugenzi ya TPA itakutana hivi karibuni kutoa uamuzi wa mwisho kuhusiana na ajira yao.

No comments:

Post a Comment